ETETA | Home juu

Habari na Matukio

imewekwa tarehe 2021-06-02

PROGRAMU YA ‘WATOTO WETU TUNU YETU’ KUWANUFAISHA WATOTO WENGI ZAIDI MKOANI MOROGORO

(Pichani ni viongozi kutoka mashirika yanayojihusisha na watoto ya CIC na CDO pamoja na viongozi mbalimbali wa Elimu Mkoani Morogoro walipotembelea wanafunzi wa darasa la awali katika shule ya Msingi Ngai iliyoko katika kata ya Mchombe Wilayani Mlimba Mkoani Morogoro tarehe 24/5/2021)    

Moja ya kitu tunachojivunia hapa kwetu Morogoro ni uwepo wa taasisi (NGOs), Mashirika na watu binafsi wanaofanya kazi kwa kushirikiana na serikali katika kuwahudumia watanzania. Unakumbuka jinsi taasisi na wadau wa elimu walivyogombania fursa ya kumwendeleza mtoto Charles Mathias aliyegundulika kuwa na kipaji katika hisabati akiwa darasa la awali huko halmashauri ya Morogoro vijijini?

Leo tutawazungumzia wadau wetu wengine wa elimu ambao kwa nafasi yao wameweza kufanya makubwa sana katika kuunga juhudi za serikali za kuwahudumia wananchi hasa katika utoaji wa elimu ya awali. Ni nani hao na wamefanya nini kuwanufaisha watoto wetu? Majibu yote ni katika aya zifuatazo.

Mwaka 2018, Shirika la kimataifa la ‘Children in Crossfire (CIC)’ lenye ofisi zake jijini Dar es Salaam kwa kushirikiana na taasisi nyingine ya wazawa ya ‘Children Development Organization, (CDO)’ ya Morogoro waliomba kushirikiana na serikali katika kutoa maandalizi mazuri ya watoto wadogo kwaajili ya kujiunga na darasa la kwanza. Mashirika yote hayo mawili yana malengo yanayofanana ya kusimamia malezi na maendeleo mazuri ya watoto wadogo kati ya miaka 3 hadi 6. CIC na CDO wanaamini kwamba ili mtoto afanikiwe katika taaluma za madarasa ya juu ni lazima ajengewe msingi bora wa malezi kupitia elimu ya awali.

Mashirika hayo hulenga zaidi maeneo ya vijijini ambako watoto wengi hukosa fursa ya elimu ya awali na kupitia changamoto nyingi zinazoathiri makuzi na maendeleo yao. Katika kutimiza wajibu wao, CIC na CDO hufanya mambo yafuatayo;

i)                   Kuhamasisha uanzishaji wa vituo vya watoto (day care centers) vya kijamii vyenye gharama nafuu kwa mzazi kulipia.

ii)                 Kutoa mafunzo ya utoaji wa elimu ya awali kwa walimu, wakuu wa shule, maafisa elimu wilaya na kata, viongozi wa kijiji, wazazi nk.

iii)               Kufadhiri vifaa vya kufundishia na kujifunzia kwa watoto wadogo kama vile makabati ya kutunzia vifaa, penseli, vitabu, michoro nk.

iv)               Kusimamia masuala ya lishe na usalama wa mtoto.

v)                  Kuboresha miundombinu ya darasa la awali.

vi)               Kulea vituo vilivyoanzishwa na kutengeneza mifumo ya kuweza kujiendesha hata baada ya wao kuondoka.

vii)             Kufanya tathmini na kushauri serikali juu ya mabadiliko au maboresho ya sera zinazosimamia watoto yanayohitajika kutegemeana na mahitaji ya wakati uliopo.

Kwa sasa CIC na CDO wanafanya kazi katika mikoa miwili pekee ambayo ni Dodoma na Morogoro.  Kwa hapa kwetu Morogoro wamekuwa wakifanya kazi katika wilaya za Mvomero, Ifakara na Mlimba tangu mwaka 2018 ambapo mradi huo unatarajiwa kukamilika mwaka 2022.

Kuanzia tarehe 24 hadi 27/5/ 2021, viongozi wa CIC na CDO walikuwa wakifanya tathmini ya mafanikio yaliyopatikana katika programu yao kwa muda wote tangu walipoanza. Miongoni mwa viongozi hao alikuwa ndugu Heri Ayubu ambaye ni Msimamizi Mkuu wa Mipango na uendeshaji pamoja na Frank Samson kutoka shirika la CIC. Wengine ni ndugu Marsel Salema na Joseph Machira ambao ni viongozi kutoka CDO. Viongozi hao waliambatana na Mwl. Wilson Anatory ambaye ni Afisa kutoka Idara ya Elimu Mkoa aliyemuwakilisa Afisa Elimu Mkoa wa Morogoro Eng. Joyce M. Baravuga.

Zoezi hili lilifanyika kwa kutembelea Wilaya za Mlimba na Ifakara na kukagua vituo vilivyokuwa vikinufaika na programu hiyo pamoja na vile visivyonufaika ili kupata ulinganifu. Pia, walizungumza na Maafisa elimu Wilaya na Kata, Maafisa wa ustawi wa jamii, kamati za shule, wazazi, walimu wakuu wa shule na walimu wa darasa la awali katika shule husika.

Shule zilizotembelewa ni pamoja na Shule ya Msingi Ngai iliyopo katika kata ya Mchombe na shule ya msingi Ngajengwa iliyopo katika kata ya Igima zote  Wilayani Mlimba. Pia walitembelea kituo cha watoto  wadogo (day care school) cha Mt. Yohana kilicho chini ya kanisa katoliki Mlimba. Shule nyingine ni Shule ya msingi Darajani iliyopo katika kata ya Mwaya Wilayani Ifakara pamoja na kituo cha watoto cha Upendo kilichopo katika wilaya hiyo.

Kwa ujumla wadau wote hapo juu walionesha kufurahia programu hiyo kwakuwa imesaidia watoto wengi kuwa katika mikono salama ya walimu badala ya kuachwa mitaani ambako hakuna uhakika wa kesho yao.

Wazazi wengi wamehamasika kuchangia maendeleo ya watoto wao na hata kushiriki shughuli ndogondogo za kuandaa zana za kufundishia watoto kwa kushirikiana na mwalimu wa darasa la awali. Kamati za shule zimeweza kujitengenezea mpango kazi unaowaongoza katika mipango yao ya mwaka ya uendelezaji wa shule na watoto. 

Walimu wa madarasa ya awali kwa kushirikiana na walimu wakuu wa shule wameweza kuboresha mandhari ya madarasa ya awali kuwa na muonekano unaoshauriwa kitaalamu kwa kupanga sehemu kuu za darasa kama vile sehemu ya kusomea vitabu, sehemu ya kuandikia, sehemu ya kucheza,  sehemu ya kufanyia sanaa nk. Pia, madarasa yamepambwa vizuri kwa picha na maandishi ya kujifunzia watoto kama inavyoshauriwa kitaalamu.

Katika majumuisho ya ziara hiyo yaliyomshirikisha Afisa Elimu Msingi halmashauri ya Mji Ifakara ndugu Sylvester Kalagile pamoja na Mwalimu Mkuu wa shule ya msingi Darajani, viongozi wa CIC na CDO walishukuru sana kwa ushirikiano walioupata tangu siku ya kwanza hadi ya mwisho katika ziara yao ya kufanya tathmini. Walionesha kufurahishwa na jinsi wazazi walivyoitikia uhamasishaji wao na kuwezesha shule kujisimamia zenyewe.

Sambamba na hilo, walitoa wito kwa viongozi wa elimu wakiwemo Maafisa elimu Wilaya na kata, walimu wakuu wa shule na wadau wengine kujifunza na kuhamisha mambo mazuri yaliyo katika shule zilizonufaika na programu kwenda katika shule zingine zisizo katika programu.  Lengo ni kuharakisha maendeleo na kuleta usawa katika shule zote kwa wakati mmoja.

Naye Afisa Elimu msingi katika halmashauri ya Mji Ifakara ndugu Sylevester aliwashukuru viongozi wa CIC na CDO kwa kuleta programu hiyo katika shule za wilaya hiyo na kuahidi kuendelea kutoa ushirikiano unaohitajika. “Nimejionea tofauti ya mwonekano kati ya darasa la awali, darasa la kwanza na la pili. Ningependa kuona madarasa hayo yakifana ili mtoto anapoingia darasa la kwanza asione tofauti kubwa kati ya alikotoka na aendako” alisema ndugu Sylvester. 

Kwa upande wake Mwl Wilson Anatory aliyemuwakilisha Afisa Elimu Mkoa wa Morogoro Eng. Joyce Baravuga alitoa shukurani kwa mashirika ya CIC na CDO kwa kuuchagua mkoa wa Morogoro katika ya mikoa miwili Tanzania iliyo katika programu yao. Zaidi aliwapongeza kwa kuamua kufanya kazi katika vijiji vilivyopo katika wilaya za pembezoni mwa mkoa wa Morogoro badala ya huduma zote kupatikana maeneo ya mjini. Zaidi aliwahakikishia ushirikiano katika kufanikisha programu hiyo na kuwaomba kupanua wigo ili kuzishirikisha shule nyingi zaidi za Mkoa mzima wa Morogoro. Aliwataka kuitumia ‘youtube channel’ ya ETETA TV inayomilikiwa na Idara ya Elimu Mkoa wa Morogoro katika kutekeleza programu yao ili taarifa ziweze kuwafikia haraka wananchi wote.

Mjadala ulihitimishwa kwamba, baada ya tathmini hiyo yatapangwa mafunzo mengine ndani ya mwaka huu 2021 kwaajili ya walimu wa madarasa ya awali, walimu wakuu wa shule, wazazi na kamati za shule, maafisa elimu kata na wengineo ili kuzifikia shule nyingi zaidi ambazo bado hazijanufaika na programu hii. Hongereni sana CIC na CDO, karibuni tena Morogoro ili kazi iendelee.

Idara ya Elimu Mkoa wa Morogoro

©2021

Soma Zaidi
imewekwa tarehe 2021-03-01

RAS, REO - MOROGORO WAMTABIRIA MTOTO CHARLES MATHIAS KUWA MHANDISI MWENYE UMRI MDOGO ZAIDI TANZANIA

Katika siku za hivi karibuni, video inayoendelea kusambaa kwa kasi katika mitandao ya kijamii ni ile ya mtoto mdogo Charles Mathias Mbena (6) aliyegundulika kuwa na kipaji kisicho cha kawaida cha kukokotoa hesabu zisizoendana na umri wake kwa kutumia kichwa chake. Hahitaji kikokotoo wala Kompyuta.

Mtoto Charles ambaye ana miezi miwili pekee shuleni akiwa amesajiliwa kama mwanafunzi wa darasa la awali/chekechea mwaka huu 2021, amekuwa gumzo mitandaoni hali iliyowavutia viongozi wakubwa na wadau mbalimbali wa malezi na elimu kufika shuleni kwake kumtia moyo na kumsaidia kuendeleza kipaji chake.

Katika video iliyoambatanishwa na makala hii, ni Katibu tawala wa Mkoa wa Morogoro Mhandisi Emmanuel Kalobelo pamoja na Afisa Elimu Mkoa wa Morogoro Mhadisi Joyce Baravuga walioambatana na viongozi na wadau wengine katika ziara ya kwenda katika shule ya Msingi Nyingwa iliyopo katika Wilaya ya Morogoro Vijijini anakosoma mtoto Charles Mathias.

Jambo linalotia moyo zaidi ni namna viongozi hao wakubwa walivyoamua kuacha shughuli zao kwaajili ya kumfikia mtoto Charles Mathias katika kijiji ambacho hata magari yao yalishindwa kupita katika baadhi ya maeneo na hivyo kulazimika kutembea kwa miguu.

Mhandisi Kalobelo aliagiza mtoto Charles kuvushwa darasa kutoka chekechea hadi darasa la kwanza wakati taratibu zaidi zikiendelea kufanyika za kumwendeleza mtoto huyo. Alisisitiza kuwa ni lazima mtoto Charles atafutiwe makao mengine yatakayokuza kipaji chake. 'Rais wetu John Pombe Magufuli kila siku anasisitiza Tanzania kuwa nchi ya viwanda, ni lazima tutambue na kuendeleza vipaji hivi ili baadaye tuwe na wanasayansi wakubwa wazawa. Si lazima wagunduzi wote watoke nje ya nchi'. Alisema Mhandisi Emmanuel Kalobelo.

Mtoto Charles alizawadiwa zawadi za kitaaluma zinazoweza kusaidia kumchangamsha zaidi akili ikiwemo mpira wa miguu, daftari na vifaa vya kuchorea.

Katibu tawala alieleza kuwa, wafadhiri wengi wamejitokeza kumsaidia mtoto Charles na hivyo kuwaomba wazazi wa mtoto huyo kutoa ushirikiano kwakuwa ni kwa nia nzuri ya kumwendeleza Charles.

Baadhi ya wafadhiri hao ni pamoja na Mkurugenzi wa Manispaa ya Morogoro (Mjini) aliyetoa nafasi katika shule maalumu ya Manispaa inayofundisha kwa lugha ya kiingereza (English medium school). Pia, Mhandisi Kalobelo alimtambulisha mwakilishi wa kanisa la Full Gospal la Dar es Salaam waliojitolea kumsomesha mtoto Charles hadi atakapomaliza elimu ya shule ya msingi.

 

Katibu tawala alimwagiza Afisa Elimu kuratibu mambo yote hayo kwa haraka inavyowezekana ili mtoto Charles asikwame.

Pia aliagiza majengo yanayoendelea kujengwa katika shule hiyo yakamilike haraka iwezekanavyo na mengine mapya yaanze kujengwa ili kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa watoto wote wanaobaki shule hapo. 'Wanafunzi nawaomba msijikatie tamaa, ni mazingira kama haya haya na sisi tumetoka hadi tumekuwa wahandisi na viongozi katika serikali'. Alisema Mhandisi Kalobelo.

Naye Afisa Elimu Mkoa wa Morogoro Mhandisi Joyce Baravuga alimpongeza Katibu tawala kama Kiongozi wa kwanza Mkubwa kufika shuleni hapo na kuahidi kumsimamia vyema mtoto Charles. 'Mimi ni Mhandisi, Katibu tawala naye ni Mhandisi; tumekuja kumtembelea mhandisi mdogo mpenda mahesabu. Ninamwombea aje kuwa mwanasayansi Mhandisi mdogo zaidi Tanzania'. Alisema Mhandisi Baravuga.

Pia waliwapongeza walimu na wathibiti ubora wa shule ambao ndio walioibua kipaji cha mtoto Charles. Zaidi aliwapongeza wazazi wa mtoto Charles kwa malezi mazuri akiahidi kuwasaidia katika kufanikisha ndoto za mtoto Charles.

Kwa pamoja, viongozi hao waliwataka walimu na wazazi kuendelea kutambua na kuibua vipaji wa watoto ili kuvilea kwa manufaa ya taifa letu la Tanzania.

Baba yake mtoto Charles Bw. Mathias Mbena aliwashukuru viongozi hao kwa kufika kijijini kwao kwaajili ya mtoto wake Charles kitendo ambacho yeye hakukitegemea kutokea. 'Nilikuwa ninaambiwa na watu wenye simu kwamba wamemwona mwanangu kwenye mitandao ya whatsap na runinga. Ninafurahi sana kuona mkifika hapa kutokana na kipaji cha mwanangu. Ninaamini kwamba akiendelezwa ataweza kuja kuwasaidia na watu wengine'. Alisema Bw. Mbena.

Kujionea tukio zima, fungua link hii https://youtu.be/aVLhSX5MHEI  

Imeandaliwa na;

Mwl. Wilson Anatory

Kilakala Sekondari

Soma Zaidi
imewekwa tarehe 2021-01-17

‘ZERO’ ZAPUNGUA MATOKEO KIDATO CHA NNE MKOANI MOROGORO

Jitihada mbalimbali za kitaaluma zinazoendelea kufanywa na wadau wa elimu ikiwemo viongozi, walimu, wazazi na wanafunzi zimeonesha kuzaa matunda bora mkoani Morogoro. Haya yamedhihirika katika matokeo ya kidato cha nne 2020 yaliyotangazwa hivi karibuni na Katibu Mkuu wa baraza la Mitihani la Taifa Dk. Charles Msonde.  

Katika kujali maendeleo ya watoto wetu, Idara ya Elimu Mkoa wa Morogoro imekuwa ikifanya tathmini ya ulinganifu wa ufaulu katika ngazi ya mkoa kwa kila mwaka matokeo yanapotangazwa.

Tathmini ya hivi karibuni ya matokeo ya kidato cha nne 2020 inaonesha kuongezeka kwa ufaulu katika daraja la kwanza hadi la nne huku idadi ya waliopata daraja sifuri ‘0’ ikipungua kwa kiasi kikubwa, ikilinganishwa na ufaulu wa mwaka 2019. Takwimu halisi kwa miaka hiyo miwili imeaninishwa katika jedwali hapo juu.

Tahimini ya jumla ni kuwa, ufaulu umeongezeka kutoka asilimia 78.82 kwa mwaka 2019 hadi kufikia asilimia 85.84 kwa mwaka 2020. Hii inamaanisha kuwa Mkoa wa Morogoro umefanikiwa kuongeza ufaulu kwa asilimia 7.02% ndani ya miezi 12 ya mwaka uliopita.

Katika upande mwingine, Idadi ya wanafunzi waliopata daraja sifuri ‘0’ imepungua kutoka 3,972 mwaka 2019 hadi kufikia 2,871 kwa mwaka 2020. Hii ni sawa na kusema kwamba, jumla ya wanafunzi 1,101 wameokolewa kutoka daraja sifuri kwenda katika daraja la kwanza hadi la nne ndani ya miezi 12 ya mwaka uliopita.

Pongezi nyingi zimwendee Mwalimu namba moja na Afisa Elimu Mkoa wa morogoro Eg. Joyce Baravuga kwa uongozi wake uliofanikisha yote haya katika mkoa wetu.  Pongezi zaidi ziwaendee viongozi wote wanaoshirikiana kwa pamoja katika kusimamia maendeleo ya elimu na watoto katika mkoa wetu akiwemo Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Loata Ole Sanare, na Katibu Tawala Mkoa wa Morogoro Eng. Emmanuel Kalobelo.

Tunawapongeza Maafisa elimu Wilaya, Waratibu elimu na Wakuu wa shule kwa usimamizi wao mzuri wa shughuli za ufundishaji na ujifunzaji mashuleni.  Pongezi za pekee ziwaendee walimu wote mnaotumia muda wenu mwingi kuwaandaa watoto kwaajili ya mitihani ya taifa inayotupatia tathmimini za maendeleo kama hizi. 

Pamoja na ufaulu huo, changamoto kuu inabaki kuhakikisha tunaondoa daraja sifuri katika matokeo ya mkoa wetu wa Morogoro. Haipendezi na haifurahishi kuona mwanafunzi aliyeandaliwa kwa miaka minne shuleni kupata daraja sifuri ‘0’ ambalo ni fedheha kwa mwanafunzi husika, mwalimu hadi mzazi wake.

Katika suala la elimu, kila mmoja wetu anahusika. Kama wewe sio mwanafunzi, inawezekana unasomesha mtoto. Serikali kwa upande wake imeamua kutoa elimu bure. Nasi tuendelee kushirikiana pamoja ili kuunga mkono juhudi hizo za serikali katika kuhakikisha kuwa kila mtoto anayezaliwa ananufaika na elimu yetu  kwa kumwepusha kupata daraja sifuri maarufu kama ‘Division zero’.

Imeandaliwa na;

Mwl. Wilson Anatory

Kilakala Sekondari

Soma Zaidi
imewekwa tarehe 2021-01-11

WANAFUNZI KILAKALA SEKONDARI WAELIMISHWA NAMNA BORA YA KUNAWA MIKONO KUEPUKA MAGONJWA YATOKANAYO NA KULA UCHAFU

Ikiwa leo tarehe 11 januari 2021 ni siku ya kwanza baada ya shule kufunguliwa kwa muhula mpya, wanafunzi wote wa kidato cha 1 hadi 6 wa shule ya sekondari Kilakala walipata fursa ya kuelimishwa namna bora ya unawaji mikono ili kuepuka magonjwa yatokanayo na kula uchafu. Hatua hii imekuja wakati mwafaka ambapo wanafunzi wameelimishwa kulinda afya zao ili kutoathiri maendeleo yao ya kitaaluma wanapoendelea na muhula mpya waliouanza.   

Akitoa maelezo ya awali, mratibu wa mafunzo hayo katika ngazi ya shule Mwl. Zena Uliza ambaye pia ni mwalimu anayehusika na malezi ya wanafunzi (Matron), alitoa ufafanuzi juu ya adhima ya serikali kudhibiti magonjwa ambayo yamekuwa yakiwapata watu wengi zaidi huku sababu zake zikiwa ni kutokana na kula uchafu utokanao na kinyesi cha binadamu (Fecal diseases).

Homa ya matumbo (Typhoid) ni miongoni mwa magonjwa yaliyotiliwa mkazo zaidi kwakuwa watu wengi wamekuwa wakibainika kuugua ugonjwa huo wanapopima hospitalini. Kwakuwa vimelea vya ugonjwa huo vinasadikika kuishi kwenye kinyesi cha binadamu, ni dhahiri kuwa mtu anapougua ugonjwa wa homa ya matumbo anaweza kuwa amekula kinyesi chake mwenyewe au cha mtu mwingine bila yeye kujua.

Hii inatokana na tabia ya kutonawa mikono au kunawa mikono kwa njia duni zisizoweza kuondoa vimelea vya magonjwa hasa baada ya kutoka chooni.  “Ifike mahali tuwe tunaona aibu kusema kwa watu kuwa tunaumwa homa ya matumbo kwasababu ni ugonjwa unaodhihirisha uchafu wetu wa kula vinyesi. Alisema Mwl. Uliza.

Wanafunzi walielekezwa kwa vitendo hatua zote za unawaji bora unaoondoa uchafu wote kwenye mikunjo ya vidole, kucha na viganja vya mikono kwa kutumia sabuni ya maji pamoja na maji tiririka.

Ilielezwa kuwa, mtu mmoja mzembe asiponawa mikono vizuri anaweza kuwasababishia ugonjwa watu wengine anaoshirikiana nao kwa njia mbalimbali ikiwemo kushikana mikono au kula pamoja. Tunapougua watu wengi kwa wakati mmoja tunarundikana kule hospitali na kuzidi uwezo wa wahudumu wa afya. Unapuuza kitendo cha dakika 2 kunawa mikono halafu unakuja kupoteza siku nzima au wiki nzima hospitalini baada ya kuugua. Katika hali kama hiyo mwanafunzi hawezi kuwa na maendeleo mazuri kitaaluma.

Itakumbukwa kuwa mara baada ya kuingia madarakani mwaka 2015, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. John Pombe Magufuli alionesha kukerwa na hali ya watanzania kuugua ugonjwa wa Kipindupindu ambao pia unatokana na vimelea vinavyoishi kwenye uchafu wa kinyesi cha binadamu. Aliamua kuahirisha sherehe za kumbukumbu ya Uhuru wa Tanganyika na kuagiza kila mtanzania kutumia siku hiyo kuhakikisha anafanya usafi katika eneo lake ili kuutokomeza ugonjwa huo.

Rais Magufuli alieleza kuwa, ni aibu kwetu kuendelea kuugua ugonjwa wa kipindupindu unaotokana na kula uchafu utokanao na vinyesi vyetu sisi wenyewe. Aliagiza viongozi wote wa mikoa kuhakikisha kuwa hakuna mtu atakayethibitika kuwa na kipindupindu katika maeneo yao. Hali hiyo ilifanikiwa na hadi sasa ugonjwa wa kipindupindu unaelekea kubaki kama historia nchini kote. Kama tuliweza kipindupindu ambacho ni hatari zaidi kwa maisha ya binadamu, tunahsindwaje kudhibiti homa ya matumbo? Kila mtu atimize wajibu wake.

Pamoja na Mwl. Uliza, elimu hiyo ilitolewa kwa ushirikiano na walimu wote wa idara ya somo la elimu ya viumbe hai (Biology) shuleni hapo Kilakala. Wanafunzi wameonesha kufurahia elimu hiyo na kukiri kuwa walikuwa wakikosea kunawa mikono yao hasa baada ya kushika uchafu. Waliahidi kuwa mabalozi wazuri kwa jamii hata baada ya kumaliza shule.

Mpango huu wa uelimishaji wanafunzi ni wa kitaifa na unatarajiwa kufanyika katika shule zote Tanzania, ili kutokomeza magonjwa yatokanayo na uzembe wetu wa kutonawa mikono ipasavyo.

Imeandaliwa na;

Mwl. Wilson Anatory

Kilakala Sekondari

Soma Zaidi

Wahisani

  • Wahisani
  • Wahisani
  • Wahisani
  • Wahisani
  • Wahisani